Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Micheal Mcharo (52) mkulima mkazi wa Kijiji cha Bendera katika wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro anadaiwa kumpiga risasi tatu Edson Shangari (59) kwa kutumia silaha aina ya bastola na kumsababishia kifo.
Tukio hilo linatajwa kutokea Desemba 26,2024 majira ya saa 9:30 asubuhi katika kitongoji cha Kaloleni kijiji cha bendera kata ya Bendera Tarafa ya Ndungu ambapo risasi zilizopigwa zilimpata marehemu katika maeneo ya mkono wa kushoto, kifuani kushoto na shavu la kushoto.
Taarifa za awali zimeeleza kuwa marehemu alikuwa anaelekea shambani kwake akiwa njiani hatua chache kabla ya kufika shambani alikutana na mtuhumiwa ambaye alimshambulia marehemu kwa kumpiga risasi tatu.
SOMA HII; Kamanda Chadema Amfokea Mbowe Hadharani
Chanzo ni ugomvi baina ya wawili hao ni mgogoro wa shamba uliodumu tangu 2022 na kwamba haukuwahi kupatiwa ufumbuzi hadi tukio linatokea na kwamba mwili wa marehemu umehifadhiziwa kituo cha afya ndugu kusubiri uchunguzi wa daktari.
Mkuu wa wilaya ya Same Kaslida Mgeni ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama ya wilaya amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba tayari mtuhumiwa amekamatwa.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro Kamishna Msaidizi Mwandamizi SACP Saimon Maigwa amesema jeshi la Polisi tayari limefanikiwa kumkamata mtuhumiwa pamoja na bastola inayoaminika kutumika katika kufanya mauaji hayo .