Mkuu wa Polisi Wilaya ya Ludewa Mkoani Njombe Selestin Luhende amewataka Wanandoa kuacha kupekua simu za Wenza wao ili kuepuka madhara yanayoweza kupatikana ikiwemo ugomvi unaoweza kuvunja ndoa pamoja na adhabu zinazoweza kutolewa kwa mujibu wa sheria.
OCD Luhende endapo Mwanandoa utabainika au kukutwa na hatia ya kupekua simu ya Mwenza wako adhabu yake kwa mujibu wa sheria ni faini ya Tsh. milioni 5 mpaka Tsh. milioni 20 au kifungo cha miaka mitano na wakati mwingine vyote kwa pamoja.
Luhende amesema hayo wakati akitoa elimu juu ya masuala mbalimbali ya usalama katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichokuwa kikiendelea Wilayani humo “Kupekua simu ya mwenza wako au kuangalia meseji zilizoandikwa ujue tayari umevunja sheria za Nchi na ukipatikana na hatia adhabu yake ni Tsh. milioni 5 au milioni 20 au kifungo cha miaka mitano au vyote kwa pamoja”
Amesema endapo utampiga Mwenza wako kwasababu ya kuangalia simu yake na kukuta jambo la kukukasirisha, jambo la kwanza kushughulikiwa ni kosa la wewe kupekua simu ya Mwenza wako.