Watu wanne wakazi wa Ifakara wilaya ya Kilombero Mkoa wa Morogoro wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kilombero kwa tuhuma za mauaji ya bodaboda aitwaye Shabani Castory Mhawile.
Washitakiwa hao ni Denis Denis Swai maarufu kwa jina la Nkane (34) mvuvi, mkazi wa kiyongwile, Athumani Said Mpango maarufu Suma (38) mkazi wa Mahema, Musa Lyanga Bushiri maarufu kama Big Popa, (28) mkazi wa upogoroni na Alhaji Hamadi Likwaya, (32) bodaboda mkazi wa hola.
Akiwasomea shtaka hilo la mauaji mahakamani hapo Wakili wa Serikali Simon Mpina mbele ya Hakimu Mfawidhi Regina Futakamba, alisema kuwa Septemba 05, 2024 huko katika kambi ya uvuvi Senga, Pori la Akiba Kilombero maeneo ya Ipatilo kata ya Minepa wilaya ya Kilombero mkoa wa Morogoro washitakiwa hao kwa pamoja walimuua Bodaboda huyo aitwaye Shabani Castory Mhawile.
Baada ya kumaliza kusoma shitaka hilo wakili wa serikali Mpina alidai kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika na washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kwasababu Mahakama haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na Hakimu Futakamba aliahirisha shauri hilo hadi Novemba 18,2024 kwaajili ya kutajwa na washitakiwa wamepelekwa rumande gereza la kiberege kutokana na kesi hiyo haina dhamana.
Katika tarehe tofauti Jeshi la Polisi Wilaya ya Kilombero walikamata watuhumiwa hao baada ya kufunguliwa kwa taarifa ya kupotea kwa bodaboda huyo ambapo katika upelelezi iligundulika kuwa watuhumiwa hao walimua bodaboda huyo kisha mwili wake kutelekeza katika Pori Tengefu la Kilombero lililopo Ipatilo na kuiba pikipiki yenye namba za usajili MC 426 EFV aina ya Hojue aliyokuwa akiendesha marehemu