Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Freeman Mbowe amesema kuna makundi yanayoratibu kufanyika mapinduzi ndani ya chama hicho na makundi hayo ndiyo yanayomsukuma Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Bara, Tundu Lissu kugombea nafasi ya Uenyekiti.
Mbowe ameyasema hayo wakati akifanya mahojiano na mtangazaji wa Crown Media Salim Kikeke na kueleza kuwa
“Kuna kundi linaloitwa diaspora (watanzania waishio ughaibuni) ni kundi dogo tu wala sio kusema ni diaspora wote wa Tanzania hili kundi dogo linalojaribu kupanga mapinduzi ndani ya CHADEMA wengine hata hatuwajui tunawaona tu kwenye majina ya mitandaoni wanajiita Tanzania Diaspora ni kundi ndani ya Diaspora”
Mbowe ameeleza kuwa zaidi ya kundi hilo kuna kikundi kingine kinachoitwa Sauti ya Watanzania ambacho kinachoongozwa na aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho Dkt. Wilbroad Silaa “kuna makundi ya watu kama Dkt. Silaa na kikundi kinachojiita Sauti ya Watanzania, Dkt. Silaa alikimbia CHADEMA mwenyewe akaenda Chama Cha Mapinduzi (CCM) akafungiwa Serena pale(Serena Hotel) baadae akahamishiwa Canada akapewa zawadi ya ubalozi.”
Mbowe ameongeza kuwa amekuwa akishangazwa na wanaomuunga mkono Lissu kuwa sio watu ambao ni wanachama kweli kweli hata hivyo anashindwa kuelewa kwa nini Dkt. Silaa hawekezi nguvu kwenye chama chake bali anawekeza muda na nguvu CHADEMA.
“Kazi aliyoifanya muda wote akiwa balozi(Dkt.Silaa) chini ya utawala wa Magufuli(Hayati Dkt. John Pombe Magufuli) ni kujaribu kuichonganisha CHADEMA na kutoa taarifa na mpaka kuandika kitabu cha uongo eti leo Dkt.Silaa ndiye anafanya kampeni ya Lissu kuchukua uongozi wa chama alisahau nini Dkt Silaa ambacho leo anakitaka”
Hata hivyo Mbowe ameongeza kuwa wengine wanaomuunga mkono Lissu ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Iringa na Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Nyasa Mchungaji Peter Msigwa ambaye kwa sasa ni kada wa CCM.