Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Iringa imemuhukumu kifungo cha miaka Minne jela Mzee Chezali Kambole 74 ambaye ni Mkazi wa Semtema kwa kosa la kumchoma na kitu chenye ncha kali ambaye anadaiwa kuwa ni mdeni wake Filbert Bai 32 mkazi wa mtaa huo huo wa semtema uliopo katika Manispaa ya Iringa.
Imeelezwa Mahakamani hapo kuwa mshtakiwa Mzee Chezali Kambole alikuwa akijishughulisha na shughuli ya kuuza mipini ya jembe ambapo alikuwa akimdai marehemu Filbert Bai kiasi cha shilingi elfu mbili.
Siku ya tukio inaelezwa kuwa wote walikuwa kilabuni na wanakunywa pombe ndipo Mzee Chezali alimkumbusha Filbert kuwa anaomba deni lake na ndipo marehemu alimjibu ‘ silipi’
Baada ya majibizano ya muda Mzee Chezali akaanza kumpiga marehemu sehemu mbalimbali za mwili wake kisha akamchoma kisu sehemu ya kushoto ya kifua hali iloyopelekea filbert kupoteza damu nyingi na kupelekea kifo chake.
Hukumu hii ya kesi ya kuua bila kukusudia ilisomwa na Jaji Angaza Mwaipopo wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Iringa na upande wa Jamuhuri ukisimamiwa na Wakili Habati Ishengoma pamoja na Majid Matitu huku upande wa mshtakiwa ukiwasilishwa na Wakili Jerry Mungo pamoja na Asifiwe Mwanjero.