Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara imewahukumu kunyongwa hadi kufa watuhumiwa wawili kati ya maofisa saba wa jeshi la Polisi waliokuwa wanakabiliwa na mashitaka ya mauaji ya mfanyabiashara wa madini Mussa Hamisi (25) mkazi wa Kijiji cha Ruponda wilayani Nachigwea mkoani Lindi.
Hukumu hiyo imetolewa Juni 23, 2025 katika Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara chini ya Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Hamidu Mwanga.
Waliohukumiwa adhabu hiyo ni Mrakibu wa Polisi, Gilbert Kalanje ambaye alikuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Mtwara na Mrakibu Msaidizi wa Polisi, Charles Onyango ambaye alikuwa Mkuu wa Kituo cha Polisi Mtwara.
Mauaji hayo yalifanyika Januari 5, 2022, huku mwili wa marehemu ukikutwa umetupwa katika Kitongaji cha Majengo Kijiji cha Hiari Wilaya ya Mtwara, ikielezwa kabla ya kuuliwa, alidai fedha zake Sh 33,748,980 ambazo maofisa hao wa polisi wanadaiwa kuzichukua kutoka kwake, wakati walipomfanyia upekuzi.
Hata hivyo mahakama hiyo imewaachia huru maofisa watano wa jeshi hilo kutokana na kushindwa kuthibitisha mashtaka, ambao ni Mrakibu wa Polisi Msaidizi, Nicholaus Kisinza ambaye alikuwa Mkuu wa Kikosi cha Intelejensia ya Jinai Mkoa wa Mtwara.
Wengine ni Mkaguzi wa Polisi, John Msuya Mganga Mkuu wa Zahanati ya Polisi mkoani Mtwara, Mkaguzi wa Polisi Msaidizi Marco Mbuta, Mkaguzi wa Polisi Shirazi Mkupa pamoja na Koplo Salimu Mbalu.